Page 1 of 2
CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM
KIGODA CHA UPROFESA CHA MWALIMU J.K NYERERE KATIKA TAALUMA ZA
UMAJUMUI WA AFRIKA
KWA USHIRIKIANO NA KITUO CHA UBIA KATI YA SEKTA YA UMMA NA SEKTA
BINAFSI (PPPC)
MAJUMUISHO YA KONGAMANO
Ndugu Washiriki wa Kongamano, kwa ruhusa yenu, napenda kuwaletea majumuisho
yanayotokana na mawasilisho, mijadala, na michango yenu katika kongamano hili.
- Tofauti na huko nyuma, Dira ya 2050 imetengenezwa kupitia ushirikishwaji mpana
wa makundi yote na imezingatia ajenda na mwelekeo wa kimataifa. Hii si Dira ya
serikali peke yake, bali ni Dira ya Taifa—Dira ya kila Mtanzania, kuelekea kujenga
jamii bora, uchumi imara na jumuishi. Kiufupi ndiyo mwelekeo mkuu wa nchi. - Kukamilika kwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 kumeweka msingi thabiti kwa
utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya 2050. Dira hii mpya imejengwa kwa nguvu
juu ya mafanikio yaliyopatikana na miundombinu imara iliyowekwa kupitia Mpango
wa Tatu wa Maendeleo (2020/21–2025/26). Kwa hivyo, maeneo yaliyotekelezwa
kwa ufanisi yanabaki kuwa nguzo muhimu katika kufanikisha malengo ya Dira ya - Ushiriki wa wananchi ni nguzo kuu ya mafanikio ya utekelezaji wa Dira ya
Maendeleo ya 2050. Mafanikio hayo hayatawezekana bila mchango wa kila
mmoja—mwananchi mmoja mmoja na makundi mbalimbali katika jamii—katika
kuibua mawazo, kushiriki maamuzi, na kufuatilia utekelezaji wa vipaumbele vya
kitaifa. - Mwelekeo wa uchumi ni msingi wa kimkakati katika kufanikisha Dira ya Maendeleo
ya 2050. Dira ya 2025 inalenga kufikia uchumi wa kipato cha kati ngazi ya juu,
hivyo maandalizi ya sera na mipango lazima yazingatie uhalisia wa uchumi pamoja
na maudhui ya Dira hiyo. Bajeti ya kwanza chini ya Dira ya 2050, ambayo
maandalizi yake yanaanza mwishoni mwa mwaka huu, inapaswa kuakisi mwelekeo
huu kwa usahihi na kwa uthabiti. - Kujenga uchumi mkubwa duniani kote hutekelezwa kupitia ushirikiano na sekta
binafsi. Vivyo hivyo, ndoto kuu zilizoainishwa katika Dira ya 2050 zitatimia kupitia
ushiriki mpana wa sekta binafsi. Ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi ni
nyenzo muhimu katika kufanikisha ndoto ya kujenga uchumi mkubwa na jumuishi.
Hili kufanikiwa linahitaji mabadiliko ya fikra juu ya ushiriki wa sekta binafsi kwenye
uchumi.
Hivyo basi, kwa kuzingatia yaliyojadiliwa, Kongamano linaazimia yafuatayo:
Mosi: Serikali imewekeza kwa kiwango kikubwa kwenye miundombinu ya
kiuchumi kama bandari, barabara na umeme. Hata hivyo, tunashauri kuimarishwa
kwa uwekezaji kupitia ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi (PPP). Hatua
hii itapunguza mzigo wa kifedha kwa serikali na kuruhusu rasilimali zaidi
kuelekezwa katika maeneo muhimu ya kukuza rasilimali watu, ikiwamo afya na
elimu kusudi kuchochea uchumi jumuishi.
Pili: Uamuzi wa serikali kutumia mikopo katika kutekeleza miradi ya maendeleo
ya kimkakati ni sahihi, kwani unalenga kuongeza tija ya kiuchumi na kuchochea
ukuaji wa taifa wa muda mrefu, hivyo kuleta uchumi jumuishi.
Tatu: Serikali imefanya uwekezaji mkubwa kukuza rasilimali watu. Hata hivyo, ipo
haja ya kupanua nafasi ya ushiriki wa sekta binafsi ili kuongeza ufanisi, uvumbuzi,
na wigo wa fursa zitakazochangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi, hivyo
kutengeneza uchumi jumuishi.
18 Septemba 2025
Mbeya
Page 2 of 2